Viashiria 15 kuwa kipaji chako kitakufikisha mbali


KIPAJI NI DHAHABU
Rafiki yangu, nimeandika kitabu. Kinaitwa KIPAJI NI DHAHABU. Ili kupata kitabu hiki, wasialiana na mi kwa 0755848391 sasa

Rafiki yangu mpendwa karibu sana kwenye makala ya siku ya leo. Na leo tunaenda kuona viashiria 15 vinayoonesha kuwa kweli hiki kipaji chako ulichonacho kinaenda kukufikisha mbali.

1. upo tayari kuanza kidogo

Kama upo tayari kuanza kidogo kisha kuendelea kukifanyia kazi kipaji chako ili kuhakikisha kwamba unakikuza na kukifikisha juu zaidi, basi hiki ni kiashiria tosha kuwa kipaji chako siku moja kitakufikisha mbali sana.

2. Unafanya mazoezi mara kwa mara

Bila kujali kuwa una kipaji kikubwa kiasi gani, mazoezi ni lazima ili uweze kukisukuma kipaji chako juu zaidi. kwa hiyo, kama una kipaji na unafanya mazoezi ya kipaji chako. Siyo mara moja na wala siyo mara mbili, bali kila siku. Basi ujue kuwa hiki kipaji chako kinaenda kukufikisha mbali kwelikweli.

3. Unapenda kujifunza

Kuna maarifa mengi yamejicficha kwenye vitabu. mtu ambaye hajifunzi na kupata maarifa mapya, ni mzee hata kama ana miaka 21 na mtu ambaye anajifunza na kupata maarifa, ni kijana hata kama ana miaka 75. Sasa wewe ni mzee au kijana? Kama wewe ni kijana, basi hiki ni kiashiria tosha kuwa unaenda kufanikiwa kwa viwango vikubwa

4. Kufanya mambo ya msingi na kuachana nay ale ambayo siyo ya msingi’

Ujue ndani ya siku kuna mambo  mengi ambayo unaweza kufanya, unaweza kuutumia muda kwenye kuchati, unaweza kuutumia muda wako kupiga soga na marafiki, unaweza kuutumia muda wako kwenye kuperuzi na mengineyo mengi. Ila kama kwa vyovyote vile unatoa muda wako na kuuwekeza kwenye kipaji chako na kufanya majukumu ambayo ni ya msingi kwako, hiki ni kiashiria tosha kwamba kwa vyovyote vile rafiki yangu, unaenda kufanikiwa kwenye kipaji chako na kipaji chako kitakufikisha mbali.

Hivyo rafiki yangu, endelea kupambana na kufanya mambo ya msingi huku ukiachana na yale ambayo siyo ya muhimu.

5. Kujihusisha na marafiki na watu chanya

CHUMA KINANOA CHUMA. Huu ni usemi ambao huwa napenda kuusema na kuusisitiza, ningependa na wewe uufahamu pia, kuwa chuma, kinanoa choma. Hivyo, wale watu ambao unakuwa unatumia muda mwingi ukiwa nao, ni wazi kuwa wewe unaenda kuchukua tabia zao. Kama muda wako mwingi unautumia ukiwa na watu ambao wananoa vipaji vyao na kuvifanyia kazi, hicho ni kiashiria kingine kuwa wewe unaenda kufanya makubwa na kipaji chako.

Nikiwa kwenye maonesho ya nanane na vitabu vyangu (2022)

6. Una malengo na unayafanyia kazi

Kama una malengo na hayo malengo unayafanyia kazi. labda ni malengo ya kufanya mazoezi, au malengo ya kujifunza, basi hiki ni kiashiria tosha kwamba unaenda kufanikiwa kwa viwango vikubwa sana. sasa swali langu kwako siku ya leo ni je, un malengo. Na je, hayo malengo unayafanyia kazi?

7. Ukianguka unainuka

Watu wengi huwa wanaanza vitu, pale wanapokutana na changamoto basi wanaachana na kile wanachofanya na hivyo kuendelea na maisha yao kama kawaida. Sikiliza rafiki yangu, changamoto ni moja ya kitu ambacho unahitaji kukifanyia kazi kwenye maisha yako. Changamoto hazijawahi kukosa kwenye maisha. Unapaswa kuzifanyia kazi, na kila unapoanguka, basi usisite kuinuka maana kuanguka ni sehemu ya maisha.

8. Unapenda kujichangamotisha

Ujue sisi binadamu hatupendi kufanya vitu vya tofauti. Mara zote huwa tunapenda kufanya vitu vilevile kwa namna ileile bila ya usumbufu wowote ule. Sasa kama unapeda kujichangamotisha na muda mwingine kuchukua hatua ambazo siku za nyuma ulikuwa hujawahi kuchukua, basi ukae ukijua kuwa hiki ni kiashiria tosha kuwa utafanikiwa sana na hicho kipaji chako.

9. Upo tayari kwenda hatua ya ziada

Wengi kwenye maisha wanapenda mabadiliko, ila hakuna ambaye yuko tayari kwenda hata hatua moja ya ziada ili kutengeneza hayo mabadiliko. Ila kama wewe unaenda hatua ya ziada na kufanya zaidi vile unavyopaswa kufanya, basi hiki ni kiashiria tosha kuwa unaenda kufanikiwa sana kwenye kile unachofanya.

10.Unajiongoza

Kuna watu wengi sana kama hawajielewi vile, ni mpaka awepo mtu wa kuwaongoza na kuwaonesha kitu gani cha kufanya, ndipo na wao wanaweza kufanya kitu. Kama hakuna mtu wa kuonesha au kuwaongoza kufanya hicho kitu, basi utakuta kwamba wale wanabweteka.

Sasa kama unaweza kujiongoza kwenye majukumu yako na kuyafanya bila hata kuhitaji usimamizi, basi ujue wazi kuwa unaenda kufika mbali  sana na hicho kipaji chako.

11. Unajikubali

Kama hujikubal, basi hakuna mtu ambaye atakukubali. Rahisi tu kama hivyo.

12. Unajali sana muda

Muda ni mali. Hili wala hata halina ubishi, kama unatumia muda wako vizuri kwenye kunoa na kuendeleza kipaji chako badala ya kufanya mambo mengine ambayo hayana manufaa, basi hiki ni kiashiria iosha kuwa unaenda kufanikiwa sana na kipaji chako na utafika mbali.

Rafiki yangu naomba utambue kwamba kwa siku tuna saa 24 tu. Sasa hizi saa unapaswa kuhakikisha kwamba umezitumia vizuri na kwa manufaa yako, kama wewe unautumia muda wako vizuri, basi hongera sana. Ila kama hautumii muda wako vizuri, basi jihoji mara mbilimbili ili kuanzia leo hii uanze kuutumia muda wako kwa manufaa na kwenye malengo na ndoto zako ambazo unafanyia kazi

13. Una kocha

Kama una kocha wa kukusimamia na kukufuatilia kwenye kile unachofanya, basi hiki ni kishiria kingine kuwa unaenda kutoboa. Asilimia kubwa ya watu wenye vipaji huwa wanakwama kwa sababu hawana msimamizi wa kuwafutilia kwa ukaribu, kitu ambacho huwa kinawafawanya wafanye vitu kwa motisha kwa siku chache na  baadaye kupoteza hiyo motisha. Ila unapokuwa na motisha na mtu wa kukusimamia nyuma yako, maana yake hata ukukikutana nchangamoto au kitu chochote, bado utajisukuma na kusongambele ili uweze kufikia malengo na ndoto zako.

14. Unapata muda wa kupumzika

Ni kweli kuwa unapaswa kupambana kwa ajili lya kuhakikisha unafanyia kazi kipaji, malengo na ndoto zako ili uweze kufikia malengo makubwa sana kwenye maisha. Ila pia unapawa kuwa na muda wa kupumzika ili usije ukafanya kazi kupitiliza mpaka ukapata burnout.

Hiki ni kitu cha msingi ambacho huwa wanakifanyia kazi watu wanaofanikiwa na vipaji vyao, na wewe ukikifanyia kazi, basi hii itakuwa ishara tosha kuwa wewe unaenda kufanikiwa na kipaji chako.

Unaweza kufanya kazi saa 18 kila siku jumatatu mpaka jumamosi, na jumapili ukapumzika na kupata muda wa kutosha wa kupumzika.

15. unajali sana mahusiano yako

Kama unajali sana mahusiano yako, mahusiano ya mwenza wako na familia yako. Basi ujue kwamba unaenda kufika mbali. Mwenza wako ni kiungo muhimu sana, kama mko sawa kwenye safari yenu ya mafanikio mtafika haraka, ila kama mnakinzana ni vigumu sana kufika.

Sasa kuanzia leo hii, hakikisha kwamba mahusiano yako na mwenza wako unayatunza vizuri ili yaweze kukaa kwa usawa.

Tofauti na hapo mimi nakutakia kila la kheri.

Umekuwa name,

Godius Rweyongeza

0755848391

Morogoro-Tz


3 responses to “Viashiria 15 kuwa kipaji chako kitakufikisha mbali”

  1. Andiko mujarabu sana hili. Nimetembelea hapa kwa mara ya kwanza siku ya leo, na nimefahamu, kwamba kuna maarifa ya kuchota. Hongera kaka Godius.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

X