Deprecated: Constant FILTER_SANITIZE_STRING is deprecated in /home/songambele/public_html/wp-content/plugins/blogger-to-wordpress-redirection old/b2w-redirection.php on line 91
JINSI UBUNIFU UNAVYOWEZA KUKUINUA KWENYE BIASHARA - SONGA MBELE

JINSI UBUNIFU UNAVYOWEZA KUKUINUA KWENYE BIASHARA


Siku moja nilikuwa naongea na rafiki yangu Edius Katamugora, akawa ameaniambia juu ya kinyozi aliyekuwa anatengeneza app ya kuwakumbusha wateja kurudi kunyolewa. Yaani, app yenyewe ingekuwa inafanya kazi hivi,

Pale Ambapo ungekuwa unaenda kunyoa kwa yule fundi kinyozi, angekuwa anachukua namba yako, saa chache baada ya kuwa umenyoa app ingekutumia ujumbe kukushukuru kwa kuja konyoa. Wakati app hiyohiyo ikikutumia ujumbe wiki mbili mbeleni ikikumbusha kunyoa kwa mara nyingine. Maana kwa kawaida Ndani ya wiki mbili nywele zinakuwa zimeshaota, kiasi cha kuhitaji kunyoa tena. Huu ni ubunifu.

Siku nyingine nilikutana na jamaa ambaye alikuwa anatunza namba Simu za wateja wanaofanya miamala kwake, siku nyingine ulipokuwa unaenda kufanya muamala kwake badala ya kuanza kukuuliza namba yako ni ipi, alikuwa anakuuliza unatuma kwenye namba ileile au tofauti. Ukisema ileile basi hapohapo alikuwa anaendelea na muamala bila kukuuliza namba yako.Huu pia ni ubunifu mwingine.

Ubunifu kwenye biasharani moja ya kitu muhimu Sana ambacho Unahitaji kulifanyia kazi. Ubunifu unawapa sababu ya wateja kuja kwenye BIASHARA yako badala ya biashara za watu wengine.

  • Unaweza Kuwa ubunifu wa KUWEKA benchi za watu kukaa.
  • Unaweza pia kuwa ubunifu wa kukumbuka kitu alichonunua mteja mara mwisho au mbacho anapendelea kununua mara kwa mara.
  • Unaweza Kuwa ubunifu wa kuwapa watoto pipi moja ya shilingi 50 kila wanapokuja kununua dukani kwako. Si unajua watoto huwa wanatumwa sana na wazazi, ukibuni kitu Cha kuwapa motisha, unashangaa kila wanapotumwa wanakuja dukani kwako kununua.
  • Unaweza kuwa mbunifu kwa kuwapa wataje wako ofa, hata ya  kitu kidogo pale wanaponunua kwako mara kwa mara.
  • Kwa vyovyote vile ubunifu Ni moja ya kitu muhimu sana unachohitaji.

Ubunifu unakutofautisha wewe na watu wengine ambao wanakuwa wanafanya kitu Cha kwako. Ubunifu unawapa watu sababu ya kuja kununua kwenye biashara yako badala ya kwenda kununua kwingine [MSISITIZO].

Na ubunifu siyo tu kwenye biashara,ubunifu unaweza kuutumia kwenye Kipaji chako, elimu yako, mahusiano, n.k. Ndio maana nimeandika kitabu Cha akili ya Diamond Kitabu kinachoeleza mambo 50 ya kujifunza kutoka kwa Dimond Platnumz Kuhusu Ubunifu, Kipaji Na Mafanikio. Unaweza kukipata kwa kuwasiliana na 0755848391

Ubunifu kwenye biashara.

Hivi ninapoandika HAPA, naendelea kusoma kitabu cha THE SCHOOL OF MONEY. Juzi wakati nakisoma nilikutana na kitu ambacho kilinifurahisha sana. Ilikuwa Ni hadithi fupi ya dereva teksi ambaye aliongeza ubunifu kwenye Kazi yake na kuanza kulipwa mara mbili mpaka mara kumi zaidi ya alivyokuwa analipwa mwanzoni.

Mwandishi anaieleza siku alivyoshuka uwanja wa mdege (airport) na kukutana na dereva huyo. Dereva yule alivyosimamisha teksi tu, wakati anaingiza mizigo ya abiria wake kwenye gari alimpa abiria wake karatasi. Kwenye karatasi hiyo kulikuwa na maono makubwa ambayo dereva huyo anayafanyia kazi na msimamo ambao dereva anausimamia kwenye uendeshaji teksi.

Kitu hiki kilimshangaza kidogo mwandishi maana hakuwahi kuona dereva wa aina hii popote pale duniani. Mwandishi wa kitabu hicho aliposoma kwenye Ile karatasi mojawapo wa kauli, ilisema lengo langu ni kusafirisha na kuwafikisha abiria kwa usalama wa hali ya juu.

Wakati mwandishi akiwa anaendelea kutafakari Hilo, dereva alikuwa amemaliza kupakia mizigo yake, na hivyo muda huohuo aliingia kwenye teksi yake.

Alivyokaa tu kabla ya kuwasha teksi kuondoka, alimwambia abiria wake huwa ana utaratibu wa kuwapa abiria wake kahawa, hivyo alimkaribisha aweze kupata kahawa.

Abiria alikataa kwa kusema hapendi kahawa Bali anapenda kinywaji Baridi. Palepale dereva akamtolea soda nzuri na kumpa yule mteja wake. Hiki kitu kilimshangaza abiria kiasi akawa anakuuliza mbona napata huduma za viwango vya kifalme?

Baadaye abiria alifunguka na kumwuliza dereva teksi, huwa unafanya hivi kwa abiria wako wote? Hapo ndipo dereva yule alijieleza kwa kusema kuwa KWELI huwa anafanya hivyo kwa kila abiria. Akaendelea kwa kueleza historia yake ya siku za nyuma.

Ambapo hapo zamani alikuwa kama madereva teksi wengine. Alikuwa analalamila kuwa maisha Ni magumu. Sasa siku moja alikaa na kutafakari kuona utofauti gani yeye anao ambao watu wengine hawana. Alichokuja Kugundua Ni kuwa yeye na madereva wengine walikuwa wanafanya kazi yao kwa mazoea.

Teksi zao wote zilikuwa chafu. Walikuwa hawachukui mawasiliano ya wateja wao baada ya kuwabeba ili waendelee kuwasiliana na endapo siku nyingine hao abiria wana safari wawasiliane nao waweze kuwasafirisha kwa mara nyingine.

Dereva huyo anasema tangu siku hiyo hakuwahi kurudi nyuma na Wala hakuwahi kufanya kazi yake kama ambavyo mtu mwingine alikuwa akifanya. Alijitofautisha.

Kitu hiki kilimfanya kwanza asiwe tu anakaaa kwenye vijiwe bila mwelekeo, maana watu wengi walikuwa wkintafute huyo dereva, na hata mwandishi kukutana na yule dereva ilikuwa ni kama bahati, siku hiyo. Maana dereva huyo yuko bize muda wote akisafirisha abiria wanaompigia na abiria wengine wapo tayari kulipia fedha yao mapema ili tu waweze kusafirishwa na yule dereva.

Huo pia ni ubunifu.
Na wewe Unahitaji kufanya ubunifu kwenye biashara yako au kitu chochote unachofanya. Wape watu sababu ya kuja kununua kwako badala ya kwenda kununua kwa mwingine.

Wape watu sababu ya kufanya biashara na wewe na siyo mwingine. kuwa mbunifu.

Ubunifu wa KUONGEZA teknolojia.

Moja ya kitu ambacho nimekuwa nikiwaambia watu wengi ni kuwa kwenye Biashara yoyote Ile unayofanya unapaswa kuangalia namna gani unaweza KUONGEZA teknolojia. Ukifuatilia Biashara nyingi zinazofanyika kwenye kipindi Cha leo, utagundua kuwa kitu kikubwa ambacho Biashara hizi zimefanya Ni KUONGEZA teknolojia au intaneti kwenye biashara ambazo zikikuwepo kwa siku nyingi zilizopita.

Watu wamekuwa wanauza na kununua vitabu Vitabu kwa siku nyingi kabla ya amazon. Walichofanya Amazon Ni KUONGEZA teknolojia au intaneti kwenye uuzaji wa vitabu. Badala ya mtu kuhangaika kurafuta vitabu umbali mrefu, Sasa anaweza kuvinunua akiwa chumbani kwake tu.

Amazon wanafanya Biashara ya kuuza vitabu, Ila Biashara ya kuuza vitabu siyo ngeni kwenye macho ya watu. Ni Biashara ambayo imekuwepo kwa siku nyingi sana ila Amazon wameipa uhai zaidi kwa kuiongezea teknolojia na intaneti.

Wewe pia kwa Biashara yako unayofanya unaweza kufanya kitu Kama hiki. Unaweza KUONGEZA teknolojia au intaneti. Huo Ni ubunifu rafiki yangu

Usiache kuchukua kitabu changu cha JINSI YA KUIBUA UBUNIFU ULIO NDANI YAKO kwa 7,000 tu/- softcopy. Hki pia kimebuniwa kwa namna ya kipekee. Na kinauzwa kwa njia ya kibunifu ya mtandao, hahaha

Ukifanya kitu unachopenda ubunifu unakuw amwingi

Kuna siku nilikuwa nikiongea na mteja wetu mmoja ambaye yuko mkoani Mara (Msoma mjini). Siku hiyo alikuwa amepokea kitabu cha jinsi ya kufikia NDOTO ZAKO na kuanza kukisoma.

Kitu cha pekee nilichopenda kutoka kwake ni usemi wake anaosema kuwa ukifanya kitu unachopenda, Ubunifu unakuwa mwingi.

Na hiki kitu nimeona nikushirikishe na wewe pia.

Kuna utafiti unaonesha kuwa watu wengi wanakufa siku ya jumatatu baada ya kula Bata wikendi halafu jumatatu wanaamka na kwenda kufanya kazi wasiyopenda. Hicho kitu tu, kinawakatisha tamaa.

Ndiyo maana nimeupenda huu usemi, kiasi cha kuwa tayari kukushirikisha huu usemi na wewe.

Ujumbe mkubwa ninaotaka kusisitiza hapa ni kuwa ukifanya kitu unachopenda, ubunifu unakuwa mwingi.

Ukifanya kitu unachopenda hutachoka Ukifanya kitu unachopenda ubunifu unakuwa mwingi.

Thomas Edison alikuwa analala saa tatu kwenye maisha yake na kuamka mapema kwenda kazini. Siku moja aliulizwa kwa nini unafanya sana kazi.

Aliwajibu watu kwa kuwaambia kuwa sijawahi kufanya kazi.

Umeona ee! Alikuwa anafanya kitu anachopenda. Hivyo, kwake hakuona kama hiyo ilikuwa kazi.

Hivi wewe unafanya unachopenda kweli? Unafanya unachopenda?

Ngoja nikukumbushe, “ukifanya kitu unachopenda, ubunifu unakuwa mwingi”.

Ubunifu Unaboresha Biashara Yako

Kama wewe umekuwa mtumiaji wa muda mrefu kidogo wa mtandao wa WhatsApp utagundua kuwa mtandao huu umekuwa unafanyiwa marekebisho ya hapa na pale kila mara. Kuna kipindi haya mambo ya status au WhatsApp business hayakuwepo.

Nakumbuka suala zima la kubold, italicize, underline na strikethrough na yenyewe hayakuwepo.

Ila kadiri siku zilivyoendelea yamewekwa. Hayo ni machache tu kati ya marekebisho mengi ambayo wamefanya.

Ninachotaka kukwambia ni kwamba kwenye biashara yako, ni vizuri kuwa mtu wa kufiria nje ya boksi na kufikiria zaidi ya hapo ilipo kwa sasa.

Ubunifu utaitofautisha sana biashara yako na biashara za watu wengine. Maana hata ukisema ufanye biashara ambayo haijawahi kufanywa hapa duniani. Ndani ya miezi sita tu, kuna watu watakuona ukiifanya na wenyewe wataanza kuifanya. Kumbe basi, kitu pekee ambacho kinaenda kukutofautisha wewe na wengine ni ubunifu.

Ubunifu Siyo Mpaka Uwe Na Wazo Ambalo Halijawahi Kuwepo

Wengi wanapofikiria ubunifu basi wanadhani, mbunifu yeyote anapaswa kuja na wazo la kipekee sana na wazo ambalo halijawahi kuonekana. Unaweza kuja na wazo la kawaida, ila kwenye biashara yako likawa linaleta mapinduzi.

Inashauriwa walau kila siku uwe unafikiria mawazo ya kawaida kumi tu na kati ya hayo utoe moja au mawili ambayo utayafanyia kazi. Ukiwa mtu wa kufikiria hivi ni uhakika kuwa mwaka mmoja baadaye, kama ni biashara, lazima tu utakuwa umeisukuma mbali.

Ubunifu Siyo Mpaka Uwe Profesa

Ubunifu ni kitu tunazaliwa nacho. Ndiyo maana utagundua kwamba kila mtoto huwa anapenda kuumba vitu mbalimbali kwa kutumia udongo, mchanga au malighafi zozote anazoona zinamfaa.

Kwa hiyo hiki kiwe kiashiria kwako kuwa UBUNIFU ni kitu tunacho, tumezaliwa nacho na tunaenda nacho popote. Kadiri ambavyo utautumia ubunifu kwenye kazi, biashara au eneo lolote, ndivyo utakavyoimarika zaidi na zaidi.

Moja kati ya vitu muhimu sana katika biashara, mahusiano na kazi ni ubunifu. Ni kupitia ubunifu mtu unaweza kuja na mbinu mpya za kuongeza wateja, ni kupitia ubunifu unaweza kujua ni bidhaa gani ukiiboresha zaidi itakuongezea wateja zaidi. Ni kupitia ubunifu utajua ni bidhaa gani ukiipunguza  au ukiiondoa kwenye mfumo wako wa biashara utakuwa hujapungukiwa na kitu. Kwa hakika binafsi nauita ubunifu moyo wa biashara.

Sasa ubunifu ni nini?

Mpaka hapa utakuwa unajiuliza huu ubunifu unaoongelewa ndio unafananaje? Ndio nini haswa?

Vyanzo mbali mbali vimeudadafua ubunifu kama matumizi ya njia bora zaidi zinazokidhi kutatua changamoto mpya, changamoto ambazo tayari zipo lakini hazijapatiwa ufumbuzi bado, au changamoto zilizopo kwenye soko au jamii kwa kipindi husika.

Hata hivyo kwa mantiki ya andiko hili, tutatumia maana ifuatavyo UBUNIFU NI HALI YA KUJA NA WAZO JIPYA LA KUBORESHA, KUIMARISHA AU KUBADILISHA KITU KATIKA NAMNA YA UPEKEE.

Ubunifu katika biashara ni wa aina mbili. Kwanza kuna ubunifu mlalo na ubunifu sambamba.

Ubunifu mlalo ni aina ya ubunifu ambapo mtu unakuwa na kitu kimoja ila unakikuza kitu hicho hicho zaidi na zaidi. Mfano mtu unagundua kwamba kalamu za aina fulani zinapendwa sana na watu katika eneo langu. Basi unaongeza uzalishaji wa kalamu za aina hiyo hiyo ili ziwe nyingi zaidi. Huu ndio unaitwa ubunifu mlalo.

Ubunifu sambamba. Huu ni ubunifu ambao unatokea pale unapokuwa unazalisha kitu kimoja ila ukagundua kwamba ili kitu hiki kifanye kazi vizuri basi hapa tunahitaji kitu kingine cha ziada. Kwa kutumia mfano wetu hapo juu. Unazalisha kalamu ila unagundua kwamba ili kalamu yako ifanye kazi vyema basi inahitaji daftari. Hivyo unaanza kuzalisha na daftari. Huu ndio  ubunifu sambamba. Ubunifu sambamba tunaweza kuuona katika maeneo mengi sana kwenye maisha yetu. Ukiangalia uwepo wa simu umesababisha uwepo wa laini za simu. Huu ni ubunifu sambamba. Uwepo wa viatu umezalisha uhitaji wa soksi huu nao ni ubunifu sambamba.

Mtu anayeuza runinga lazima tu atatakiwa kuwa na remote na hata ving’amuzi, huu pia ni ubunifu sambamba.

Jinsi ya kutumia aina hizi mbili za ubunifu.

Bila shaka mpaka hapo utakuwa unajiuliza, hivi hizi aina mbili za ubunifu zitanisaidiaje kwenye biashara zangu?

Jibu ni rahisi sana. Kama kuna biashara yako unafanya sasa hivi. Angalia ni bidhaa gani inapendwa zaidi na watu. Ukishaipata bidhaa ya namna hii basi izalishe zaidi na hakikisha unaongeza mauzo. Kumbuka mapato makubwa sana kwenye biashara yako hayatoki kwenye kuuza kila kitu. Ila yanatokea kwenye kuuza bidhaa chache kwa wingi sana. Sasa hapa unahitaji kukaa chini na kujiuliza ni bidhaa gani hizi chache ambazo nikizizalisha kwa wingi zitaongeza mapato makubwa sana.

Au ni bidhaa gani nikiziongeza kwa wingi kwenye mzunguko bado nitazidi kuuza sana. Hapa utakuwa umetumia ubunifu mlalo.

Unaweza pia kutumia ubunifu wima kwa kuangalia aina ya bidhaa ambayo ukiizalisha itakuwa inaendana na ile ambayo ulikuwa hapo awali. Jiulize ni bidhaa gani inaweza kwenda sambamba na bidhaa ninayouza sasa hivi na ikauza vizuri bila shida? Mfano rahisi sana ni pale unapokuwa unauza majiko ya gesi. Unaweza kuongeza kitu cha ziada kwa kuuza vyombo vingine vinavyotumika jikoni. Ukiweza kuvijua vitu hivi vinavyoenda sambamba na ile bidhaa ya awali baasi hapo utakuwa umetumia ubunifu sambamba.

Kwani kuna ulazima wa kutumia ubunifu kwenye biashara?

Zama zimebadilika, maisha nayo yamebadilika, lakini pia mfumo wa uendeshaji wa biashara umebadikika.

Katika zama za sasa biashara zinazoendeshwa kibunifu ndizo biashara zinazopendwa na watu. Kwa hiyo ubunifu sio tena suala la hiari, ni lazima. Tungekuwa kwenye miaka ya 50 na 60 kabla uhuru ambapo maduka na wafanyabiashara walikuwa wachache sana, hapo suala la ubunifu tungeliweka pembeni na kushughulika na mambo mengine. Ila kwenye zama hizi hapa hakuna jinsi ubunifu ni lazima.

Lazima kuwepo na sababu za kwa nini watu waje kununua kwako na sio kwa rafiki yako mwenye duka na anauza bidhaa kama unazouza. Sasa hapo ubunifu ndipo unaingilia katikati. Kwa hiyo ubunifu ni lazima wala sio ombi!

Ubunifu ni muhimu kwenye biashara, michezo, sanaa, uigizaji, ufundishaji, mziki, upambaji n.k. yaani maisha na ubunifu ni vitu ambavyo hatuwezi kabisa kuvitenganisha 

Sasa kama ubunifu ni muhimu kwa nini watu sio wabunifu?

Mbali na kwamba tumeona ubunifu ni muhimu sana kwenye biashara na maisha ya kawaida bado ubunifu haujapewa kipaumbele hata kidogo kwenye bara la Afrika. Kuna watu wengi sana wamezaliwa na vipaji vikubwa sana vya kubuni na kuja na mbinu mpya ila bado hawajavitumia. Hizi hapa ni sababu zinazofanya watu wafanye vitu kwa namna ile ile kila siku bila kuongeza thamani za kibunifu.

1.  KILA MTU ANAFANYA HIVYO

Mara nyingi sana watu wapo katika mazingira ambayo kila kinachofanyika basi kinafanyika kwa namna ile ile tu.

Yaani kwamba ameamka asubuhi, ameoga na kuzunguka  huku na kule, na kila mtu anafanya hivyo basi na yeye anaishi hivi. Maisha haya hayawezi kuzalisha wabunifu wakubwa. 

2. BABU ZETU WALIKUWA WANAFANYA HIVI

Hivi ushawahi kuthubutu kufanya kitu ukasikia mtu anakwambia “usifanye hivyo, babu zetu hawakuwahi kufanya kitu kama hicho“. Yaani watu wanatengeneza sheria zao wenyewe, wanazipitisha wao wenyewe na kutaka ziwe sheria za watu wote.

Sasa kwamba baba au babu alikuwa anafanya vile ina athari gani na mimi nikifanya kwa namna nyingine. Maneno haya yanatumiwa sana na watu ila kiukweli ni kwamba hata hayajengi na hayana mantiki. Hivyo ni vyema kabisa kwa wewe kama wewe kujua kwamba tunapaswa kubuni na kuja na mbinu mpya za kibunifu kila wakati.  Kuendelea kufanya vitu kwa namna ile ile kila siku hakuwezi kukuinua na kutusogeza mbele Tanzania na Afrika nzima kiujumla. Nipo nafikiri kama Albert Einstein angeendelea na fikra zile zile za mababu wetu walikuwa wanafanya hivi angeweza kugundua sheria MC²?

Hivi kama Mark Zuckerberg angeendelea kushikilia imani ya kwamba babu zetu walikuwa wanawasiliana hivi, angeweza kuja na mtandao wa kijamii wa facebook. Ebu watanzania badilikeni kabisa. Achana na mambo ya babu zetu walikuwa wanafanya hivi au vile. Sasa zama zimebadilika, maisha nayo yamebadilika hivyo na wewe unahitaji kubadilika, kubuni na kuja mbinu mpya zitakazoisaidia jamii. Acha ya kale yaitwe ya kale ila sasa panga mambo mapya ya kibunifu.  

3. KELELE ZA DUNIA

Tunaishi kwenye dunia yenye kelele nyingi sana. Kuanzia asubuhi utasikia miziki inapigwa kila kona, magari yanapita kwenye maeneo yetu ya kazi, watu wanaongea na kupiga kelele. Yaani ni vurugu mechi.

Bila ya mtu kuamua kuthubutu kujitenga na dunia kwa muda ili kutulia na kujitafakari basi maisha yataendelea hivi hivi tu. Kutokana na hali  hii basi hapa mtu unahitaji muda wa kupumzika, kujitenga na watu na kufikiri kwa kina juu ya maisha yako, biashara, mahusiano n.k hapa ndipo unaweza kuja na mawazo mapya ya kuendeleza na kuibua ubunifu wako

4. UOGA

Hivi watu watanichukuliaje? Hili ni swali lililo kwenye akili za watu walio wengi sana. Hii ni kutokana na ukweli kwamba mtu alikuwa amezoeleka kwa namna ya kawaida kwa watu na yeye tayari amehajijengea picha ya namna hiyo kama vile ni kweli. Ingawa sio. Huu uoga huu sio wa kuendekeza hata kidogo. Vijana wa Tanzania na Afrika, umefika wakati wa kuchukua hatua kubwa sana na kuhakikisha kwamba tunaibua ubunifu ulio ndani yetu.

5. UKOSEFU WA VIPAUMBELE

Watu wengi huwa hawana utaratibu wa kupangilia kazi wanapoamka asubuhi.  Hivyo kujikuta wanafanya kazi kwa mazoea. Kufanya kazi kwa mazoea hakuwezi kuleta ubunifu kazini. Hivyo wewe kama mbunifu unahitaji kutenga muda kidogo wa kuhakikisha unafanya kitu kwa kukiboresha zaidi na zaidi.

Usijifanye umebanwa kiasi kwamba huwezi kuangalia ni kitu gani bora zaidi unaweza kufanya ili kuboresha biashara au kitu chochoe unachofanya.

Na hili litawezekana kama utapangilia ratiba yako kila siku unapoamka.

Haya ndio mambo matano yanayoua ubunifu katika bara letu la Afrika na haswa Tanzania yetu. Ukiyaepuka haya rafiki yangu nina hakika utakuwa mbunifu mzuri kwenye eneo lako la kazi, biashara, michezo kutaja ila vichache.

Hatua tatu za ubunifu

Ubunifu hupitia katika hatua mbalimbali mpaka kitu kinapokuja kuonekana. Sio tu suala la kulala na kuamka ukisema mimi ni mbunifu.

Ukizipitia hatua hizi utakuwa mbunifu mzuri sana katika dujinia hii.

1. Hatua ya kwanza ni kutambua. Hii inaweza kuwa ni

  • Kujitambua wewe mwenyewe. Wewe ni nani? Kitu gani ambacho unaweza kukibuni? Ujuzi gani ulio nao unaweza kukuogezea ubunifu ukawa bora zaidi!
  • Kutambua kile unachohitaji, (je unahitaji kubuni nini? Mwonekano wake ukoje? Je,mwonekano unaweza kubadilika baadae? Kitu gani kinakusukuma wewe kusema hivyo?

2. KUKIFANYIA KAZI. (ACTION)
Ukishatambua wewe ni nani?
Kitu gani unahitaji ili kuwa bora zaidi. Sasa hatua inayofuata ni kufanyia kazi kile kilicho ndani yako. Kuhakikisha kwamba unakiboresha. Hapa utahitaji kutumia nguvu na muda wako kubadili kile kilicho akilini mwako. Kama akilini mwako kuna mawazo hakikisha kwamba unayafanyia kazi.Yaweke katika matendo.

Soma Zaidi; Vitu Utakavyojifunza Kwenye Kurasa Za Kutoka Sifuri Mpaka Kileleni

3.Matokeo

Angalia kile kinachofanya kazi na kile ambacho hakifanyi kazi.

kinachofanya kazi endelea nacho. Kisichofanya kazi achana nacho.

Tukutane siku nyingine kwenye makala ya kuelimisha na kuhanasisha kama hii.


Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

X