Kitu kikubwa na muhimu kwenye ujasiriamali siyo kujua kutengeneza bidhaa


Kitu kikubwa na muhimu kwenye ujasiriamali siyo kujua kutengeneza bidhaa. Siyo kabisa! Ingekuwa hicho ndio kitu kikubwa basi wengi wangekuwa wametoboa.

Hiyo ni sehemu ndogo tu…

Juzi tu hapa nilikuwa naongea ndugu mmoja ambaye anakaribia kuhitimu chuo. Kama ilivyo kawaida yangu nilimwuliza una mpango gani na maisha baada ya chuo…!

Hili ni swali ambalo nimewauliza vijana wengi walio chuoni na wale ambao wanaokaribia kuhitimu kila ninapopata nafasi.

Kijana huyu alinijibu kuwa alipata nafasi ya kujifunza ujasiriamali. Si unajua ujasiriamali siku hizi watu unahusishwa na kutengeneza bidhaa kama vile sabuni, vitenge, viatu vya kimasai…..

Ukiwa unatengeneza hivyo vitu, wewe ni mjasiriamali. Kama hutengenezi hivyo vitu wewe siyo mjasiriamali. Hii ni maana potofu kweli kuhusu ujasiriamali!!!!!

Hata hivyo wacha kwanza niendelee kueleza lililonileta hapa. Inshallah, kesho au kesho kutwa nitarudi hapa kueleza mjasiriamali ni nani? Kwa mara ya kwanza nitakupa maana inayojitosheleza kuhusu mjasiriamali!

Niendelee au nisiendelee….

Acha tu niendelee hata kama hupendi 😂😂.

Sasa bwana, nataka nikwambie wewe kuwa ujasiriamali siyo tu kutengeneza hizo bidhaa. Hiyo ni sehemu ndogo sana….

Muziki mkubwa wa ujasiriamali upo kwenye kuuza bidhaa na brand ya biashara yako.

Ngoja nikwambie kitu…

Walau si unamfahamu Bakhresa. Huyu jamaa anauza hata mandazi. Ila haya mandazi yake yanasambaa kila kona ya Tanzania.

Na wewe mtaani kwako Kuna mama anatengeneza mandazi. Si ndiyo? Tena ninavyojua utamalizia kwa kusema mama yule anapika mandazi matamu kuliko ya Bakhresa!

Ila sasa usije ukakimbilia kununua mandazi kwa sababu nimeyataja hapa ukaacha kusoma makala hii mpaka mwisho. Nikikugundua…😂😂.

Sasa unadhani kwa nini maandazi ya mama hayajafika mbali hivyo?

Hapo issue kubwa ni masoko na kuuza. Na hapo ndipo ulipolala ujasiriamali wenyewe.

Ujasiriamali siyo tu kutengeneza bidhaa, bali kuziuza pia.

Usipojua namna bora na nzuri ya kuuza bidhaa hizi, utahangaika kutengeneza bidhaa nzuri ambazo wewe mwenyewe utashindwa kuziuza. Hivyo basi, ukiachana na kujifunza utengenezaji wa bidhaa. Ukiachana na kutengeneza hizo bidhaa…

Uuzaji wa bidhaa ni kitu muhimu sana na wewe unapaswa kuhakikisha unaufahamu wa ndani wa huu ujuzi.

Kama unashindwa kuuza bidhaa fanya hivi.

  1. Kaajiriwe sehemu ambapo utafanya mauzo ili ufanye mauzo kwa vitendo.
  2. Kachukue bidhaa ya mwingine na uiuze.
  3. SOMA vitabu vya mauzo na yafanyie kazi yale unayojifunza.

Kwa leo kutoka hapa Morogoro mji kasoro bahari, sina la ziada.

Umekuwa nami rafiki yako
Godius Rweyongeza
0754848391
Cheers!


Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

X